AS Vita: Simba maneno mengi, subirini dakika 90 muone!

Muktasari:

Nahodha wa AS Vital, Jackson Lunanga amesema, wapo Tanzania kwa ajili ya kusaka pointi tatu ambazo zitawapeleka hatua inayofuata ya robo fainali.

NAHODHA wa AS Vital, Jackson Lunanga amesema wamekuja kucheza fainali na Simba na dakika tisini ndio zitaamua nani mbabe wa mwenzake.


Lunanga amesema, wapo tayali kupambana na timu yoyote,  wanawaheshimu Simba ni timu kubwa lakini wao wana timu bora zaidi.


Amesema, wapo Tanzania kwa ajili ya kusaka pointi tatu ambazo zitawapeleka hatua inayofuata ya robo fainali.


"Tumewaona Simba walipokuja Congo tukacheza nao, pia tumetumia video za michezo yao mingine kuwasoma hivyo tutatumia mapungufu yao tuliyoyaona ili tupate matokeo mazuri,"alisema.

"Tunachokiomba zaidi ni mchezo wa haki tu, lakini kuhusiana na maandalizi tumejiandaa vizuri na tupo tayali kwa ajili ya mapambano tunawaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi kushuhudia mchezo huu."


Amesema, anaamini mchezo huo utakuwa mzuri na wa ushindani kutokana na kuwa ni wa fainali, kila timu inasaka tiketi ya kufuzu hatua inayofuata.