22 Azam waifuata Mtibwa Sugar

Muktasari:

Azam FC inaongoza msimamo wa Ligi Kuu msimu huu ikiwa na pointi 21 ilizokusanya katika mechi zake saba dhidi ya timu za Polisi Tanzania, Coastal Union, Mbeya City, Prisons, Ihefu, Kagera Sugar na Mwadui

Jumla ya nyota 22 wa Azam FC wameelekea mkoani Morogoro kwa ajili ya mchezo wao wa raundi ya nane ya Ligi Kuu dhidi ya Mtibwa Sugar utakaochezwa Jumatatu, saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Jamhuri.

Taarifa iliyotolewa na Ofisa Habari wa Azam FC, Thabit Zakaria 'Zaka Zakazi' imefafanua kuwa msafara wa timu hiyo ulioelekea Morogoro una jumla ya wachezaji 22 ambapo makipa ni wawili, mabeki nane, viungo watano na washambuliaji saba.

"Kikosi cha wachezaji 22 cha Azam FC kimeondoka Dar es Salaam  mchana wa leo kuelekea Morogoro ajili ya mchezo wa raundi ya nane dhidi ya Mtibwa Sugar.

Kabla ya safari, timu ilifanya programu ya mazoezi asubuhi katika Uwanja wa Azam Complex ," alisema Zakaria.

Wachezaji hao 22 wa Azam ambao wameelekea Morogoro kuvaana na Mtibwa Sugar ni makipa Benedict Haula na David Mapigano wakati mabeki ni Nico Wadada, Abdul Hamahama, Yakubu Mohamed, Daniel Amoah, Aggrey Morris, Bruce Kangwa, Emmanuel Charles na Abdallah Kheri 'Sebo'

Viungo ni Salum Abubakar, Frank Domayo, Mudathir Yahya, Ally Niyonzima na Never Tigere wakati washambuliaji ni Iddy Selemani, Obrey Chirwa, Richard Djodi, Andrew Simchimba, Thiery Akono Akono, Ayoub Lyanga na Prince Dube.

Azam inaivaa Mtibwa Sugar ikiwa inaongoza msimamo wa Ligi na pointi zake 21 ilizokusanya baada ya kupata ushindi katika mechi zote saba ilizocheza wakati Mtibwa Sugar iko nafasi ya 14 na pointi zake nane.