TMK kutoa shoo ya jasho

Muktasari:

Mashabiki wa Yanga wajiandae kuona shoo la maana kutoka kundi la TMK, katika hitimisho la wiki la Mwananchi, litakalofanyika kesho Jumapili kama alivyowaahidi msanii wa bongo fleva, Juma Nature.

MSANII wa bongo fleva, Juma Nature 'Sir Juma Nature' amesema anaamini mashabiki wa Yanga, watapata shoo kali kutoka kwao katika kuhitimisha kelele cha tamasha la wiki ya Mwananchi, litakalofanyika Uwanja wa Mkapa, kesho Jumapili jijini Dar es Salaam.

Kundi la TMK litapiga shoo katika tamasha la wiki ya Mwananchi, likiwa na Sir Nature, Mheshimiwa Temba na Doro,ambapo wataungana na mastaa wengine akiwemo Konde Boy ambaye anaonekana kupata kibali zaidi kwa mashabiki wa Yanga.

Sir Juma Nature amesema wamejipanga kufanya shoo itakayoleta amsha amsha kwa mashabiki kufurahia wiki yao,ambayo itaambatana na kukijua kikosi chao kitakachofanya kazi msimu unaoanza Septemba 6.

"Wajiandae kuona mapanga shoo, wanaume tukipiga kazi jukwaani siku hiyo, kwani tutahakikisha wanaondoka wakiwa kifua mbele wakiamini wana kikosi ambacho kitaendelea kuwapa furaha kwa msimu huu,"

"Ukiachana na shoo ambayo tutaifanya, Yanga msimu huu ina kikosi kizuri, ina vijana wengi ambao wana nguvu ya kufanya kazi, tunaenda kuwapa hamasa yakuwafanya waone umuhimu wao wa kukitumikia kikosi hicho,"amesema.

Amesema mashabiki wa Yanga wana sababu yakujidai siku ya hitimisho ya wiki la Mwananchi, kwani itawapa morali wachezaji wao kuona umati utakaofurika unahitaji kuona furaha msimu huu.

"Sapoti yao ni muhimu, unajua mtu yoyote anapoungwa mkono katika kazi yake, anakuwa anapata moyo wakujituma kufanya makubwa zaidi, hivyo uwingi wa mashabiki wa Yanga, kesho Jumapili utakuwa furaha kwa kikosi chao kuona watu waliopo nyuma yao,"amesema.