Nakos, Gongo la Mboto wazichapa

Licha ya kucheza na kumaliza raundi nane, mabondia Hussein Itaba na Paul Kamata lakini mabondia hao wakarudiana kuzichapa kavu kavu nje ya ulingo.

Mabondia hao wanaotoka kambi ya Nakos ya Mabibo na Gongo la Mboto kwa bondia wa zamani, Mbaruku Heri wamejikuta wakichapa kavukavu dakika chache baada ya pambano lao la utangulizi kuwasindikiza Dullah Mbabe na Twaha Kiduku kumalizika kwenye uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam usiku huu.

Katika pambano hilo, Itaba anayetokea Nakos alishinda kwa pointi za majaji 2-1., wWaliposhuka ulingoni wakiwa wanaelekea kwenye vyumba vya kubadilishia nguo, mabondia hao walianza kutambiana kabla ya kurushiana ngumi, Kamata akiwa amevua glovu, tukio lililochukua takribani dakika tano, kabla ya walinzi uwanjani kulizima.

Bondia Mada Maugo aliyekuwa msaidizi wa ulingo 'second' wa Kamata alidai chanzo cha vurugu hizo ni Itaba ambaye alimfuata Kamata na kumwambia atampiga tena, ingawa Itaba alisema si kweli.

"Mabondia wa Manzese hawana maana, huyu Itaba kaamua tu kuanzisha vurugu, ngumi zenyewe hajui," alisema Maugo.

Itaba alisema mpinzani wake alimtolea maneno ambayo si mazuri, lakini akaomba radhi kwa mashabiki wake ambao wamemsapoti na kuwa naye bega kwa bega na kushinda pambano hilo.