Beki Yanga atua Namungo

Muktasari:

Beki Jaffar Mohammed amejiunga na Namungo tayali kwa kuitumikia msimu ujao akitokea Yanga baada ya kusaini mwaka mmoja.

NAMUNGO FC imeendelea kukisuka kikosi chake baada ya leo Ijumaa kukamilisha usajili wa beki, Jaffar Mohammed kwa mkataba wa mwaka mmoja.

Jaffar alikuwa anacheza Yanga amejiunga na timu hiyo kwa ajili ya kuitumikia kwenye mashindano mbambali wanayotarajia kushiriki ikiwemo Ligi Kuu Bara na michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika.

Namungo ilipata nafasi hiyo baada ya kushika nafasi ya pili kwenye fainali za Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) ambapo ubingwa ulichukuliwa na Simba.

Usajili wake unaenda kuongeza nguvu eneo la ulinzi kwa lengo la kuhakikiaha wanakuwa imara zaidi kuelekea mashindano hayo.

Akizungumza na Mwanaspoti Online leo Ijumaa Agosti 14, 2020, Jaffar amesema ni mapema kuzungumza lolote hivyo anawaomba mashabiki wake wasubiri nini atakifanya msimu mpya ukianza.

"Ni kweli nimejiunga na Namungo baada ya kumalizana na Yanga sina mengi ya kuzungumza kwa sasa vitendo vitazungumza baada ya ligi kuanza," amesema.

Jaffar ni miongoni mwa wachezaji waliomaliza mikataba Yanga na kupewa mkono wa kwekheri.