Mayanga aanza kazi Prisons

UONGOZI wa Tanzania Prisons, umeachana na kocha wao Adolf Rishard baada ya mkataba wake kumalizika na kumpa mkataba Salum Mayanga ambaye tayari ameanza kazi leo Ijumaa.

Prisons wameanza rasmi mazoezi leo Ijumaa Agosti 14, 2020 kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara huku Mayanga akianza kazi baada ya kumaliza mkataba wa kuifundisha Ruvu Shooting ambao wamemwajiri Boniface Mkwasa.

Habari kutoka ndani ya uongozi wa Prisons, zinasema kuwa Mayanga amesaini mkataba wa miaka miwili kukitumikia kikosi hicho.

"Amesaini sio muda mrefu kuitumikia timu yetu kwa mkataba wa miaka miwili, baada ya aliyekuwepo kumaliza mkataba wake,"

Ameongeza kuwa; "Baada ya kumalizana naye ataanza majukumu yake ya kusajili kikosi atakachoona kitamfaa kufanya nacho kazi msimu ujao,"

Mayanga mbali na kuifundisha Ruvu, amewahi kuzifundisha Mtibwa Sugar, Kagera Sugar, JKT Tanzania, Mbao FC pamoja na Taifa Stars ambapo Prisons hii ni mara yake ya pili kuifundisha.