Kilimanjaro Queens yatinga fainali Challenji kibabe

BAO pekee lililofungwa dakika ya 90, likifungwa na Asha Rashid 'Mwalala' limewapeleka fainali ya Kombe la Chalenji kwa Wanawake timu ya taifa Kilimanjaro Queens, mchezo huo wa nusu fainali umechezwa Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es Salaam.

Bao hilo lilifungwa kwa shuti kali pasi ikitoka kwa Mwanahamisi Omary 'Gaucho' aliyekokota mpira kutokea upande wao wa kushoto.

Kutokana na matokeo hayo, Kilimanjaro Queens watacheza na Kenya mechi ya fainali Jumatatu saa10:00 wakati mshindi wa tatu atacheza Uganda ambao wamepigwa na Kili Queens dhidi ya Burundi waliofungwa na Kenya utachezwa saa 7:45 mchana.

Kocha wa Kilimanjaro Queens, Bakari Shime alizungumza huku wa Uganda, Faridah Belega akigoma kuzungumza na kusema: "No Comment's."

Faridah aliingia kwenye chumba cha habari na kusisitiza msimamo wake huo wa 'no comment' licha ya waandishi tofauti kumuuliza maswali.

Shime alisema: "Nimefurahi kutokana kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji wangu pia wapinzani wangu walijua mbinu nilizoingia nazo wakatuzuia."

Alisema, kitendo cha wachezaji wa Uganda kujidondosha mara kwa mara kilipunguza kasi ya mchezo.

"Walitumia mbinu hiyo ili kupoozesha mchezo lakini mwisho wa siku tumemaliza na matokeo," alisema Shime.
Mbali na Kilimanjaro Queens, Kenya, Uganda,  Burundi timu zingine zilizoshiriki ni Sudan Kusini, Ethiopia, Djibouti na Zanzibar.