Mbao, Mbeya City zapigwa nyumbani

Muktasari:

Uwanja wa nyumbani umeonekana kuwatesa Mbao kutokana na kupoteza mechi nyingi tofauti na wanapokuwa ugenini.

MBAO FC imeendelea kupoteza mechi za nyumbani baada ya leo Jumamosi kukumbana na kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Azam FC, mechi hiyo imecheza uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa.

Mbali na kuendeleza matokeo mabaya kwenye uwanja wake wa nyumbani, pia imezidi kuwa wanyonge kwa wapinzani hao kwani kati ya mechi saba walizokutana imepoteza michezo minne, sare mbili na kushinda mmoja.
Katika mchezo huo, Azam walianza kwa kasi wakihitaji kupata mabao ya mapema na kufanikiwa kwenda mapumziko wakiongoza kwa bao hilo lililodumu hadi dakika za mwisho lililofungwa na beki wao Yakoub Mohamed dakika ya 15.

Mbao walijaribu kulazimisha mashambulizi na kubahatika kupata penalti ambayo ilipigwa na Waziri Junior dakika ya 25 baada ya kuangushwa eneo la hatari na Agrey Morri, hata hivyo penalti hiyo haikuzaa bao.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi hasa Mbao wakionekana kuhitaji bao la kusawazisha lakini umakini katika umaliziaji mipira ya mwisho ulikuwa mdogo na kusababisha mchezo huo unamalizika na wao kuangukia pua.

Kwa matokeo hayo Mbao wanabaki na alama zao 14 baada ya kucheza mechi 12, huku Azam wakifikisha pointi 16 na kupanda hadi nafasi ya sita wakiwa wameshuka dimbani mara nane.
Wakati Mbao ikilala nyumbani, huku Mbeya City ambayo pia mwenendo wao si mzuri kwenye ligi imejikuta ikilala uwanja wa Sokoine jijini Mbeya dhidi ya Singida United bao 1-0, bao hilo limefungwa na Emmanuel Maziku.