Atletico Madrid yamduwaza Ronaldo na Juventus yake

Muktasari:

Cristiano Ronaldo ameshindwa kuipa pointi tatu Juventus katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Atletico Madrid.

Madrid, Hispania. Ndoto ya Cristiano Ronaldo, kupata pointi katika ardhi ya Hispania imegonga mwamba baada ya timu yake ya Juventus kuambulia pointi moja.

Nguli huyo alirejea kwa muda Hispania baada ya kudumu kwa miaka tisa Real Madrid akiwa na matumaini ya kuipa ushindi Juventus, lakini aliduwazwa na Hector Herrera.

Juventus ‘Kibibi Kizee’ cha Turin ikiwa na matumaini ya kupata pointi tatu ugenini, iliduwazwa kwa kulazimishwa sare ya mabao 2-2.

Herrera aliyetokea benchi, alifunga bao la kusawazisha dakika ya 90 na kuipa pointi moja Atletico Madrid inayonolewa na nyota wa zamani wa Argentina Diego Simeone.

Ingawa Ronaldo hakufunga katika mchezo huo, lakini alikuwa tishio kwa mabeki wa Atletico Madrid.

Winga wa zamani wa Chelsea, Juan Cuadrado na Blaise Matuidi walifunga mabao hayo kabla ya Stefan Savic na Herrera kuzima ndoto za mabingwa hao wa Italia.

Kiungo mpya Aaron Ramsey alicheza mechi ya kwanza tangu alipotua Juventus akitokea Arsenal katika usajili wa majira ya kiangazi.

Juventus itaikaribisha Leverkusen Oktoba Mosi wakati Atletico Madrid itasafiri kwenda Russia kuvaana na Lokomotiv katika mechi ya Kundi D.