Di Maria apiga mbili PSG yaichapa Real Madrid

Muktasari:

Mchezaji mpya wa Real Madrid, Eden Hazard, alianza vyema, lakini baadaye alionekana akipambana kuisaidia timu yake kupata ushindi.

Paris, Ufaransa. Angel di Maria, amewaduwaza waajiri wake wa zamani Real Madrid baada ya kuwatungua mabao mawili katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Di Maria jana usiku alikuwa nyota wa mchezo huo wa Kundi A ambao mchango wake ulichangia Paris Saint Germain (PSG) kuichapa Real Madrid mabao 3-0.

Mchezaji huyo wa kimataifa wa Argentina, alionyesha ubora wake dhidi ya wapinzani wake licha ya kudumu Makao Makuu  Bernabeu kwa misimu mitano kabla ya kujiunga na Manchester United.

Haikushangaza winga huyo mwenye kasi aliyecheza takribani mechi 200 Real Madrid kutangazwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Mchezaji mpya wa Real Madrid, Eden Hazard, alianza vyema, lakini baadaye alionekana akipambana kuisaidia timu yake kupata ushindi.

Licha ya PSG kutokuwa na nyota wake watatu Neymar, Edinson Cavani na Kylin Mbappe, lakini timu hiyo ilicheza kwa nidhamu dakika zote 90.

Mechi nyingine za jana,  Blugge na Galatasaray zilitoka suluhu,  Olympiakos ilitoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya Tottenham Hotspurs, Bayern Munich iliichapa Red Star 3-0, Dinamo Zegreb iliinyuka Atalanta 4-0, Manchester City iliigagadua Shakhtar 3-0.