Ben Pol: Nafanya kazi ya muziki bila presha

Muktasari:

Ben Pol hatishiki na ushindani uliopo sokoni kwamba anaamini kazi zake zina ujumbe ambao unawahusu mashabiki zake hivyo akitokea nyimbo itawagusa.

Dar es Salaam. Kama ulidhani mwanamuziki Bongo fleva, Ben Pol amefulia basi utakuwa umechemka, amesema bado yupo na ataendelea kutesa kwenye gemu la muziki.

Ben Pol ametoa nyimbo mpya aliyomshirikisha Nyati Mchoya inayoimbwa kwa maneno ya Kiswahili na Kigogo, ametaja maudhui yake kwamba imebeba elimu ya mambo mbalimbali katika jamii.

Alisema bado anaendelea kufanya muziki na anaona ana nafasi kubwa mbele ya mashabiki wake na kwamba hana wasiwasi wowote juu ya ushindani uliopo.

"Katika video ya nyimbo hiyo nimewashirikisha wanawake wa makamu kutokana na ujumbe wenyewe kwani nawaamini wanaweza wakafanya vitu vikubwa katika jamii."

"Bado ninapokelewa kwa shangwe na mashabiki zangu, ushindani uliopo haunisumbui kutokana na nyimbo zangu zinaishi na zinakuwa na ujumbe wa kujifunza kwa wale ambao nawapelekea"

"Nina kazi nyingi ambazo nitaziachia muda wowote kuanzia sasa, naamini zitafanya vyema, kabla ya kuimba nimefanya utafiti wa kitu gani kinafaa kufanyika," alisema Ben Pol.