Mo Ibrahim: Namungo tutafanya maajabu msimu huu

Muktasari:

Ushindi raha asikuambie mtu, Namungo FC kuanza kwa kushinda mechi mbili, kimempa kiburi kiungo wa timu hiyo, Mo Ibrahim kuona timu yao itakuwa mwiba dhidi ya wapinzani wao kwenye ligi.

Dar es Salaam. Kiungo wa Namungo FC, Mohammed Ibrahim 'Mo Ibrahim' amesema pamoja na timu hiyo kucheza kwa mara ya kwanza katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, anaamini itakuwa mwiba dhidi ya wapinzani.

Katika mechi mbili iliyocheza Namungo FC imeanza vyema ikiishinda Ndanda na Singida United, jambo linalompa matumaini Mo Ibrahim kuona timu yao itakuwa na ushindani dhidi ya kongwe katika ligi.

MO Ibrahimu alisema kwa ushindi walioanza nao, unawapa kujiamini kuendelea kupambana kuhakikisha wanajitengenezea mazingira mazuri mapema.

"Hakuna kitu kizuri kama wachezaji kuwa na ari ya mchezo, naamini Namungo itathibitisha kwa matendo kwamba haikupanda kwa bahati mbaya."

"Timu inapokuwa inashinda ndivyo wachezaji wanakuwa na hamasa ya kuendelea kutamani kufanya vizuri zaidi, tumeanza kwa kushinda dhidi ya Ndanda na Singida, hilo kwetu limetuongezea mwendo," alisema.

Mo Ibrahim amejiunga na Namungo FC akitokea Simba ambako alikuwa na changamoto ya kuanza katika kikosi cha kwanza chini ya kocha Patrick Aussems.