Makame wa Yanga apania makubwa msimu huu

Muktasari:

Kama kuna kitu anakiamini kiungo wa Yanga anayefanya vyema kwa sasa, Abdul Aziz Makame ni nidhamu, kujifunza na bidii kwamba ndio vitakavyomuwezesha kufanya maajabu msimu huu.

Dar es Salaam. Kiungo wa Yanga, Abdul Aziz Makame amesema nidhamu, kujituma na kujifunza kila wakati kutoka kwa kocha na wachezaji wenzake ndio siri inayomfanya acheze kwa kujiamini anapopewa nafasi.

Makame alionyesha kiwango cha juu katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa kati ya Yanga dhidi ya Zesco ya Zambia, akitawala vizuri eneo la safu ya kiungo.

Makame alisema msimu huu anataka kuonyesha kipaji chake ili kutimiza ndoto yake ya kucheza soka la kulipwa katika siku za usoni.

Kutokana na uwezo wake ameiitwa katika kikosi cha Taifa Stars tangu Etienne Ndayiragije alipochukua jukumu hilo.

"Soka ni kazi ninayotamani ibadilishe maisha yangu, lazima nifanye bidii ili kazi yangu iwe na thamani ya kukifikia kile ninachokifikiria kwenye maisha yangu"

"Yanga ni klabu kubwa ina wachezaji wenye uzoefu lazima nijifunze vingi kupitia kwao na kile ambacho kocha Mwinyi Zahera anatakiwa nikifanye"

"Naamini hata kuitwa kwenye timu ya Taifa inatokana na kile ambacho nimekionyesha kwenye klabu yangu ya Yanga, natamani uwe msimu wenye mafanikio makubwa kwangu" alisema Makame.