Mwanariadha Kamworor atikisa dunia Half Marathon

MWANARIADHA Geoffrey Kamworor kagonga vichwa vya habari nchini na duniani baada ya kuweka rekodi mpya ya dunia katika mbio za Copenhagen Half Marathon juzi Jumapili.
Afisa huyo wa polisi alivunja rekodi ya awali iliyodumu toka 2018 kwa kuipunguza kwa sekunde 17.
Kamworor alitumia dakika 57 na sekunde 59 kuivunja rekodi ya awali ya dakika 58:18 iliyowekwa na Mkenya Abraham Kiptum mwaka jana kwenye Valencia Half Marathon.
Akizungumzia rekodi hiyo, Kamworor ambaye ni bingwa mara tatu wa dunia katika mbio hizo, aliiitaja rekodi mpya kuwa zawadi kwake kutoka kwa Mungu.
“Nimeshinda mataji mengi mno ikiwemo World Half Marathon mara tatu na mashabiki wangu waliishi kuniuliza ni lini nitaivunja rekodi ya dunia. Nimekuwa nikiwaambia ipo siku na mwishowe Mungu kanizawadia nayo. Ni matokeo speshio sana kwangu,” kasema Kamworor.
Copenhagen half Marathon itasalia kuwa mji spesheli sana kwake Kamworor kwani ndiko alikoshinda taji lake la kwanza la dunia 2014. Alifanikiwa kutetea ubingwa wake kwenye Cardiff World Half Marathon 2016 na kisha kuitetea tena kwenye Valencia World Half Marathon 2018.