Kumbe huyu Molinga waYanga ni balaa unaambiwa

Muktasari:

Molinga amesajiliwa na Yanga msimu huu akitokea FC Renaissance Du Congo, huku akionekana kuwa mwili kibonge na hajaonyesha makeke yoyote kwa mechi kadhaa alizopewa kucheza na kufanya mashabiki kuamini Yanga imepigwa.

Dar es Salaam. WALE wanaombeza, straika mpya wa Yanga David Molinga ‘Ndama’ a.k.a Falcao wasome hapa, kwani mmoja ya mabosi walisaidia kuiboresha katika eneo la mbele msimu huu amefichua jamaa ni mtu wa kazi sema tu kwa sasa amekuwa chii...chii..chibongee!
Molinga amesajiliwa na Yanga msimu huu akitokea FC Renaissance Du Congo, huku akionekana kuwa mwili kibonge na hajaonyesha makeke yoyote kwa mechi kadhaa alizopewa kucheza na kufanya mashabiki kuamini Yanga imepigwa.
Hata hivyo, Meneja wa winga mpya wa Simba, Deo Kanda, aitwaye Nestor Mutuale  ameliambia Mwanaspoti anamjua Molinga na sio mchezaji wa kudharauliwa kwani ni mtu anayejua vyema kazi yake ya kufunga tofauti na anavyochukuliwa.
Mutuale alisema ameshtuka kuziona picha ya straika huyo zinazomwonyesha ameongezeka uzito, lakini baso sio mtu wa kubezwa pale atakapokuwa uwanjani kwa sababu ni msumbufu kwa mabeki na kuwatesa makipa.
“Namjua vyema Falcao (Molinga) sio mchezaji mdogo ni kama Deo tu, namjua kabla ya kurudi Congo msimu uliopita alikuwa kule Angola ni mshambuliaji mzuri,” alisema Mutuale.
Bosi huyo alisema mbali na kujua kufunga pia Molinga anajua kupambana kwa kutumia nguvu huku akiwa na uzoefu wa kutosha.
“Kuna wakati hapo wakati namleta Deo (Kanda) nilisikia kuna watu walisema mzee nikacheka, hata huyu nawaambia anajua kufunga na pia anajua kupambana na nguvu akitumia mwili wake mtaona akiwa sawa.”
MSIKIE ZAHERA
Kocha Mwinyi Zahera alisema jana kabla ya mechi yao na Township Rollers nchini Botswana, Molinga amemwacha nchini lakini ana ratiba nzito ya mazoezi kuanzia gym mpaka uwanjani.
“Hatukusafiri naye yupo hapo anafanya mazoezi maalum alichelewa mazoezi ya mwanzo sasa anatakiwa kujiandaa zaidi kuna ratiba nimemuachia akiietekeleza mtamuona,” alisema Zahera.