Udhamini Vodacom waitega Yanga

Muktasari:

Vodacom imekuwa ikitumia nembo yenye rangi nyekundu na nyeupe wakati Yanga imekuwa ikitumia jezi zenye rangi za kijani, njano na nyeusi.

SHIRIKISHO la Soka  Tanzania (TFF) limetamba kuwa halitokuwa tayari kuruhusu klabu yoyote kugomea kutumia nbo ya mdhamini mpya wa Ligi Kuu na litachukua hatua stahiki kwa itakayofanya hivyo.
Kauli hiyo imetolewa na Rais wa TFF, Wallace Karia wakati wa hafla ya kutangaza Mdhamini Mkuu wa Ligi Kuu ambaye ni Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania.
"Mkataba wetu wa udhamini una masharti yake ambayo tunatakiwa kuyafuata na hatutoruhusu yeyote kwenda kinyume nayo.
Masharti hayo ni kama kitabu cha Msahafu na kila mmoja anapaswa kuyafuata. Yeyote ambaye hatoyafuata tutamtoa kwenye familia yetu," alisema Karia.
Ikumbukwe kwamba timu iliyowahi kugomea kuweka nembo ya mdhamini wa Ligi Kuu miaka ya nyuma ilikuwa ni Yanga ambayo haikuwa tayari kuweka nembo yenye rangi nyekundu na nyeupe ya Kampuni ya Vodacom pindi ilipodhamini kwa awamu ya kwanza.
Mgomo huo wa Yanga ulipelekea Vodacom kuiruhusu klabu hiyo ibadili nembo yake na kuiwekea rangi za kijani na njano ambazo zinatumiwa na Yanga.