Pep afunguka sababu za kushikana masharti na Aguero

Muktasari:

Tukio hilo, lilitokea dakika ya 66 ya mchezo huo mara baada ya Guardiola kumtoa Aguero na nafasi yake kuingia Gabriel Jesus, wakati akitoka wawili hao walionekana wakitupiana maneno.

London, England. Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola  amefafanua tukio lililotokea kati yake na mshambuliaji wake, Sergio Aguero  alipomtoa  katika mchezo wa  Ligi Kuu England  dhidi ya   Tottenham uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Tukio hilo, lilitokea dakika ya 66 ya mchezo huo mara baada ya Guardiola kumtoa Aguero na nafasi yake kuingia Gabriel Jesus, wakati akitoka wawili hao walionekana wakitupiana maneno.

“Aguero aliamini nilimkasirikia kwa goli tulilofungwa. Nilihitaji kuona kila mmoja akiwa anakaba. Nimecheza soka na alitakiwa kuwa pale ili kuzuia,” alisema kocha huyo.

Guardiola aliongeza “sina chuki naye ni kati wa wachezaji ninaowapenda, niliona anatakiwa kuingia mchezaji mwingine ndio maana niliamua kumfanyia mabadiliko na sio vinginevyo.”

Kwa namna ya tukio lilivyokuwa Aguero baada ya kutoka uwanjani alionekana akitupishiana maneno na Guardiola kwa sekunde 44 kabla ya msaidizi wake Mikel Arteta kuja haraka kuwaamua.

Lakini hata hivyo wawili hao walionekana wakikumbatiana baada ya Jesus kufunga bao la tatu kwa Manchester City kabla ya mwamuzi wa mchezo huo, Michael Oliver kulikataa kufuatia uamuzi ya usaidizi wa Teknolojia ya VAR.

Mabao ya Manchester City kwenye mchezo huo yalifungwa na  Aguero kabla ya kutolewa na Raheem  Sterling huku ya Tottenham yakifungwa na Erick Lamela na Lucas Moura  aliyeingia kuchukua nafasi ya Harry Winks.