KMC yaanza kujianda mapema kwa penalti dhidi ya AS Kigali

Muktasari:

Katika mchezo wa kwanza uliopigwa Rwanda timu hizo zilitoka sare 0-0 hivyo katika mchezo wa marudiano ni lazima mshindi hapatikane hata kwa mikwaju ya penalti.

Dar es Salaam.KMC imeanza mazoezi rasmi ya kujianda na mikwaju ya penalti kuelekea katika mchezo wao wa marudiano wa Kombe la Shirikisho dhidi ya AS Kigali unaotarajia kuchezwa Agosti 23-25.

Katika mchezo wa kwanza uliopigwa Rwanda, Kigali timu hizo zilitoka sare 0-0 hivyo katika mchezo wa marudiano yanahitajika matokeo ya kumvusha mmojawao.

Baada ya kumalizika mazoezi ya KMC yaliyokuwa yanafanyika kwenye Uwanja wa Bora, Kijitonyama timu hiyo ilimalizia kwa kupiga mikwaju ya penalti kwa wachezaji wao wote.

Kocha mkuu Jackson Mayanja alionyesha kuwa makini kwa kila mchezaji kufunga penalti hizo.

Makipa Dennis Richard, Jonathan Nahimana na Juma Kaseja walikuwa wakizicheza penalti hizo kwa umakini.

Awali kocha Mayanja alikuwa akiwataka wachezaji wake kukaba kwa upande wa mabeki na washambuliaji kuhakikisha wanawatoka mabeki hao.

Zoezi hilo lilichukua takribani dakika 10 kwa kuangalia kwa umakini namna ambavyo linakamilika kwa ufasaha.

Baada ya zoezi hilo, Mayanja aligeukia upande wa faulo na alikuwa akiwapanga mabeki kucheza faulo, huku akilisimamia.

Mara baada ya kumaliza kusimamia upande wa mabeki, aliwapanga washambuliaji na viungo nao aliwataka waweze kufunga kwa kutumia mipira hiyo ya faulo.

Kocha Mayanga alizidi kuwapa mazoezi ya mbinu wachezaji wake na kuamia katika upande wa wachezaji wake kupiga mashuti bila kutuliza.

Zoezi hilo lilikiwa haliangalii beki wala mshambuliaji, kwani wote walihitajika kupiga mashuti makali kwenda golini.