Harmonize ampa zawadi ya gari Q.Chief

Muktasari:

Msanii Harmonize ampa zawadi ya gari Q.Chief ikiwa ni moja ya njia ya kuthamini mchango wake kwenye muziki

Dar es Salaam. Msanii kutoka lebo ya WCB, Harmonize amempa zawadi ya gari Toyota Porte mwanamuziki Q Chief.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Julai 22, 2019 Harmonize amesema ameguswa na maisha anayoishi Q Chief kwa sasa na kuona ana kila sababu ya kusaidiwa ikiwemo kuwa na usafiri.

Harmonize alisema hata leo alipokuwa akienda katika mkutano huo uliofanyika hoteli ya Hyatt Regency, alitumia usafiri wa bodaboda na kumuomba amlipie atakopofika jambo lilimuumiza moyo.

Msanii huyo mkali wa kibao cha Niteke, Never give up, alienda mbali zaidi na kueleza kuwa Q.Chief amekuwa kati ya msanii aliyemvutia kuingia kwenye muziki na kueleza siyo yeye tu wapi na wasanii wengine wakubwa waliong'aa kupitia yeye.

"Leo mpaka unaona wasanii wanaendesha magari, wanamiliki majumba kutokana na muziki na moja ya watu waliowavutia na walikuwa wakicopy nyimbo zao ni pamoja na Q.Chief na mimi nilikuwa mmoja wapo niliyekuwa nikiandika hadi kwenye daftari," alisema Konde Boy.

Mbali ya kumpa gari pia wametegeneza nyimbo tatu pamoja ambazo zinaachiwa leo saa 1:00 jioni na kuomba jamii impokee.

Aidha kwa vyombo ambavyo havipigi nyimbo zake, ameomba kwa Q.Chilla wazipige kama njia ya kumrudisha katika soko la muziki.

Q.Chilla alisema hakuamini kama kuna watu wanamthamini kiasi hicho hadi kuamua kumpa gari.

"Nimejikuta nalia machozi ya furaha, kwani kitendo alichokifanya Harmonize ni cha kiungwana sana angeweza kuwasaidia wengine, lakini naona anisaidie mimi," alisema msanii huyo.

Alisema pamoja na kutumia usafiri wa umma wakati maisha yake yameenda kombo anashukuru hakuwa akijisikia vibaya kwa kuwa hajawahi kuishi maisha ya kuigiza hivyo alikubaliana na kila hali.