Kocha Simba aisifu Gor Mahia kumnasa kipa Kisu

Muktasari:

Kisu aliwahi kuichezea Njombe Mji kabla ya Singida United, amejiunga na mabingwa hao wa Kenya kwa kusaini mkataba wa miaka mitatu, utakaomalizika kipindi kama hiki 2022.

Dar es Salaam.Kocha wa zamani wa Simba na  Black Leopards  ya Afrika Kusini , Dylan Kerr amesema  Gor Mahia ‘K’Ogalo’, limelamba dume kumsajili kipa wa  Mtanzania David Kisu kutoka  Singida United.

Kerr alisema K’Ogalo wamefanya usajili wa maana kwa kumsajili Kisu ambaye atawaletea changamoto ya namba, Boniface Oluoch, Fredrick Odhiambo na Shaban Odhoji.

Kocha huyo ambaye alimnoa Kisu pindi akiwa Simba alisema, “Ni kipa mzuri ambaye umri wake bado mdogo, anayeweza kuisaidia klabu.”

“Anatabia nzuri, alikuwa akifundishwa na Idd (alipokuwa naye Simba) na kwa sasa atakutana na Willis Ochieng, atakuwa bora zaidi.”

Kerr  ambaye  aliinoa Gor Mahia  na kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Kenya (KPL) , 2017 aligomea mkataba mpya na kuamua msimu uliopita kujiunga na  Black Leopards.

K’Ogalo wapo katika harakati za kutaka kukiboresha  kikosi chao baada ya kuondokewa na  mchezaji wao muhimu,  Francis Kahata  ambaye amejiunga na Simba ya Tanzania na Jacques Tuyisenge  aliyetimkia, Petro Atletico ya  Angola.

Hata hivyo, imewanasa wachezaji  wengine  sita  wapya mbali na  Kisu ambao ni  Tobias Otieno, Abdalla Shura, Elvis Ronack, Curtis Wekesa, na  Dennis Oalo huku Dickson Ambundo akiwa kwa mkopo akitokea Alliance ya Mwanza.