Kakolanya: Stars ipo kwenye mikono salama Misri

Muktasari:

Makipa waliopo katika kikosi cha Taifa Stars ni Aishi Manula wa Simba wengine ni Metacha Mnata wa Mbao ya Mwanza na Aron Kalambo wa Tanzania Prisons ya Mbeya.

Dar es Salaam. Kipa mpya wa Simba, Beno Kakolanya anaamini timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ ipo kwenye mikono salama ya makipa walipo kikosi hicho.

Fainali za  32  za  AFCON  zitafunguliwa rasmi  Ijumaa ya Juni 21 kwa mchezo wa  ufunguzi  kwenye uwanja wa  El Qahira El Dawly  kati ya wenyeji Misri dhidi ya Zimbabwe anayoichezea kiungo wa Yanga, Thaban Kamusoko.

Makipa waliopo katika kikosi cha Taifa Stars ni Aishi Manula wa Simba wengine ni Metacha Mnata wa Mbao ya Mwanza na Aron Kalambo wa Tanzania Prisons ya Mbeya.

Kakolanya alisema ubora wa makipa waliopo katika kikosi hicho ni mkubwa kinachotakiwa ni kuwa na maelewano mazuri na mabeki wao.

“Siku zote makipa huwa tunategemeana na mabeki kuna muda wao hufanya makosa basi huwa tunayasawazisha na hata sisi hufanya makosa na wao wakiwa katika mazingira kusawazisha hufanya hivyo.

“Eneo la kujilinda huwahusisha wote. Nilitamani kuwa sehemu ya kikosi cha timu ya taifa lakini   yaliyotokea kipindi cha kati yalipoteza matumaini yangu ila naamini nitarejea nikiwa bora zaidi,” alisema kipa huyo.