Kilomoni: Sijafukuzwa Simba

ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini la Klabu ya Simba, Hamis Kilomoni amesema uwepo wake katika hafla ya Kubwa Kuliko iliyoandaliwa na klabu ya Yanga haimaanishi kwamba amefukuzwa Simba.
Kilomoni alifika ukumbini hapa na kuamsha hisia za wanachama baada ya kuona kama ameamua kujiunga Yanga.
Alipopewa nafasi ya kuzungumza alisema uwepo wake ukumbini hapo ni kutokana na undugu uliopo katika timu hizo mbili.
"Vijana wa sasa hivi ndio hamjui tu umuhimu wa hizi timu, zamani mtu wa Yanga akifa anazikwa na mtu wa Simba na hata ikitokea kwa Simba basi mtu wa Yanga ndio anamzika," alisema.
Hivi karibuni Kilomoni alikuwa anapinga udhamini wa tajiri Mohammed Dewji katika klabu ya Simba na sasa amekuwa gumzo baada ya kusema hati ya majengo ya Simba anayo yeye na hawezi kuitoa.
Akizungumzia timu hizo alisema ndio muhimili mkubwa wa soka nchini kiasi cha kutenganisha watu katika pande mbili tofauti.
"Mlichokifanya Yanga ni kitu kizuri sana, kwasababu hizi ndio timu za zamani katika soka letu, hivyo mnapokuwa mnafanya jambo kubwa kupongezwa ni lazima," alisema Kilomoni.