Kabwili kumbe ana hesabu zake

Muktasari:

Kabwili aliyesajiliwa na Yanga kwa mkataba wa miaka mitano msimu uliopita akitokea Serengeti Boys

Dar es Salaam.Kipa Ramadhani Kabwili mjanja sana. Kipa chipukizi huyo wa Yanga amesema msimu uliopita ulikuwa kama darasa kwake na kuweka wazi kwamba ligi ijayo itakuwa kipimo cha kazi yake kutaka kujua anaelekea wapi.

Kabwili aliyesajiliwa na Yanga kwa mkataba wa miaka mitano msimu uliopita akitokea Serengeti Boys, amesema mashabiki wake wanapaswa kutambua alijiunga na klabu hiyo na a kukutana na makipa wazoefu wa hali naye kujitofautisha nao akijifunza vitu vingi.

"Mbali na kuwa chini ya makipa wazoefu, lakini kocha Mwinyi Zahera alikuwa akinipa nafasi ya kucheza, nilipambana kwa kadri nilivyoweza kutumia vyema nafasi niliyopewa."

Amesema anaamini kwa kile alichokivuna msimu uliopita ni wazi utamsaidia kwenye msimu ujao wa Ligi Kuu na mechi za kimataifa.

"Sio siri nisingeweza kulinganishwa na watu kama Beno Kakolanya aliye kwenye kiwango cha juu, kwani mbali na kucheza Yanga amepita pia Taifa Stars na Prisons, huku Klaus Kindoki kwao alicheza timu tofauti za Ligi Kuu," amesema.

Amesema kutoka ana hilo msimu ujao kwake anauchukulia kuwa wa changamoto zaidi na kujiandaa kufanya kazi na kipa yoyote ambaye watamsajili viongozi wake.

"Nimejitathimini nilichokifanya msimu ulioisha, sasa kazi kubwa ni kujipanga kwa ajili ya ushindani msimu ujao ili mchango wangu kuwa mkubwa na wakutegemewa ndani ya klabu," amesema kipa huyo aliyeshiriki Fainali za Afcon U17 2017 akiwa na Serengeti.

Mbali na hilo alizungumzia mashindano anayoandaa mtaani yanayujulikana kama Kabwili Cup, kwamba yanalenga kuonyesha vipaji vilivyopo chini ili viweze kujulikana na timu za ligi kuu.

"Soka lipo kwenye damu yangu, hakuna mchezaji ambaye hajatoka chini hata Ulaya historia za mastaa ambao wanatikisa ulimwenguni wametoka chini, naamini ipo siku wapo ambao watafika mbali kupitia michuano hiyo,"alisema.