Tshishimbi asaini miaka miwili Yanga

Muktasari:

Dili la Mkongomani huyo,  lilichukua saa tano hadi kukamilika jana, kutokana na kuwa kwenye makubaliano ya awali na klabu moja ya Afrika Kusini.

KIUNGO wa Yanga, Pappy Kabamba Tshishimbi amesaini mkataba mpya wa kuendelea kuwatumikia wababe hao wa Jangwani.
Dili la Mkongomani huyo,  lilichukua saa tano hadi kukamilika jana, kutokana na kuwa kwenye makubaliano ya awali na klabu moja ya Afrika Kusini.
Kutokana na hali hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Frank Kamugisha alikutana na mabosi wenzake akiwemo Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela ili kuhakikisha dili hilo linakamilika fasta.
Tshishimbi amesaini mkataba wa miaka miwili chini ya Mwanasheria mpya wa klabu hiyo, Abdullah Lyana.
Mara baada ya kusaini, Tshishimbi alisema:
“Mambo yanaanza kubadilika Yanga na ndio sababu nimebaki hapa. Kwa sasa naangalia mbele zaidi na natambua nina kazi kubwa ya kuifanya kwenye timu yangu msimu ujao.”