Viporo vyaanza kumtia presha Kocha Aussem, Coastal yajipanga kuiduwaza Simba

Muktasari:

Simba baada ya kutolewa katika Ligi ya Mabingwa sasa inaanza kupambana katika ligi ikiwa na mechi nyingi mkononi

Tanga. Kocha wa Simba, Patrick Aussems ameanza mchecheto kutokana na ratiba ngumu ya mechi za viporo vya Ligi Kuu inayowakabiri mabingwa hao watetezi.

Kocha Aussems amesema ni wazi mfululizo wa mechi hizo unahitaji mikakati itakayoiwezesha kutoka na ushindi wa kila mechi.

"Ni mechi nyingi kwa mfano timu ya Yanga imetupita michezo nane tunapaswa kuhakikisha tunaimaliza kwa kutoka na ushindi nashukuru wachezaji wapo fiti" alisema Aussems.

Naye nahodha wa Simba, Mohamed Hussein alisema baada ya kutolewa na TP Mazembe wamejipanga kuhakikisha wanatetea ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania bara.

"Tunaelekeza nguvu zetu kwenye ligi kuu tutahakikisha tunamaliza viporo vyote pamoja na michezo mingine iliyobaki kwa lengo la kutetea ubingwa wetu"alisema Mohamed Hussein

Kuhusu mchezo wao wa keshokutwa Jumatano dhidi ya Coastal Union, Mohamed Hussein alisema kwa kutambua kwamba ipo nyumbani Watacheza kwa umakini ili Kupata ushindi.

"Tunaiheshimu Coastal Union kama tulivyoiheshimu TP Mazembe, tutacheza kwa umakini ili Kupata pointi tatu.

Kocha wa Coastal Union, Juma Mgunda alisema pamoja na mashabiki wanaona mechi dhidi yao na Simba itakayochezwa Jumatano ni ngumu lakini anaamini watashinda mchezo huo.

Kocha huyo alisema Coastal Union inaiheshimu Simba, lakini mchezo wa kesho Coastal Union itatoka na ushindi.

Coastal Union hadi sasa imecheza michezo 32 ikiwa na alama 41 ambapo mlinda mlango wa timu hiyo Hussein Sharif alisema wamejiweka sawa kuhakikisha wanashinda dhidi ya Simba.