AliKiba nusuru azichape na mwamuzi kisa kupewa kadi njano mchangani

Muktasari:

Mwanamuziki na mchezaji wa Coastal Union, Ali Kiba ndiye alikuwa kivutio kwenye mechi ya michuano ya kombe la Ng'ombe kati ya Mjimuni na Wanasta.

Dar es Salaam. Hii sio ndoto ni kweli mwanamuziki na mchezaji wa Coastal Union, Ali Kiba nusura azichape na mwamuzi Ruge Mutahaba wakati timu yake ya kitaa Wanasta ilipopokea kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Mjimuni katika mechi ya kuwania kombe la Ng'ombe hatua ya makundi ilichezwa Uwanja wa Toto Tundu uliopo Tabata Segerea.

Sakata hilo lilianza AliKiba kutoka nje ya uwanja kwenda kubadilisha viatu bila ridhaa ya mwamuzi Mutahaba anayetambuliwa na DRFA.

Kutokana na kitendo hicho mwamuzi Mutahaba bila kujiuliza kujali ustaa AliKiba akamlima kadi ya njano iliyomfanya nyota huyo kuanza kumkaba mwamuzi.

Mwamuzi Mutahaba alisema kilichokuwa kimemchefua Kiba ni baada ya kumwambia mambo yake ya ustaa yawe nje ya dimbani ndani ya uwanja lazima azingatia sheria 17 za mpira.

"Kiba sijui alikuaje siku hiyo maana alikuwa na vituko ambavyo sikuweza kuvivumilia mpaka kuna wakati nilimwambia nitamtoa nje kabisa, unajua nimesomea saikolojia ya kwenda na watu wa kitaa.

"Najua kujiweka kwenye mazingira salama kwani nimechezesha sana mashindano kama hayo najua changamoto zake ndio maana nikiwa dimbani sitaki mizaha kabisa," alisema mwamuzi huyo.

Wachezaji wa timu pinzani walionekana kumkamia Kiba ambaye alionekana kushangiliwa na nyomi ya mashabiki ambao walikuja kumshuhudia akicheza.

Baadhi ya mashabiki walionekana kazi yao ni kumwangalia Kiba alikuwa akikosea ama kufanya maufundi walikuwa wanamshangilia kwa kwenda mbele.

Wakiwa wanasubiri mechi imalizike ili wapige picha na Kiba kwa kuwa timu yake ilikuwa imefungwa mabao 2-0 alienda moja kwa moja kwenda kwenye gari yake na kuwaacha mashabiki wakinung'uka wakidai nje na mpira ni wadau wa muziki wake.