Ni suala la muda Zidane ndani ya Real Madrid

Muktasari:

Zidane anajivunia rekodi yake ya kutwaa mataji matatu mfululizo ya Ligi ya Mabingwa akiwa na Real Madrid

Madrid, Hispania. Klabu ya Real Madrid muda mfupi ujao inatarajiwa kumtangaza rasmi Zinedine Zidane kuwa kocha wa kikosi hicho.

Zidane anarejea Real Madrid tangu alipojiuzulu miezi 10 iliyopita baada ya kuipa mafanikio katika Ligi Kuu Hispania na Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Nahodha huyo wa zamani wa Ufaransa, anarejea Real Madrid kujaza nafasi ya Santiago Solari aliyeshindwa kupata mafanikio tangu alipotwaa mikoba.

 Kocha wa zamani wa timu hiyo, Jose Mourinho alikuwa mmoja wa makocha waliotajwa kurejea Santiago Bernabeu, lakini jina la Zidane limeonekana kuchomoza.

Rais wa Real Madrid Florentino Perez leo alitarajiwa kukutana na bodi ya klabu hiyo kukamilisha mchakato huo.

 Zidane anarejea katika klabu hiyo akionekana shujaa baada ya kuipa mataji matatu ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Kocha huyo alindoka Real Madrid majira ya kiangazi baada ya kutofatiana na Perez kuhusu mpango wa kuwekeza msimu huu.

Awali, Zidane aliwahi kuhusishwa na mpango wa kujiunga na Chelsea kujaza nafasi ya Maurizio Sarri au Manchester United baada ya kumfukuza Mourinho.