Juma Nature amuaga Zilla kivingine

Muktasari:

Godzilla alikuwa ni miongoni mwa wasanii wanaosifika kwa kufanya Freestyle (mitindo huru) kipindi cha uhai wake.

Dar es Salaam.Wakati wasanii wengine wakiendelea kupost katika kurasa zao za mitandao jamii na kuelezea hisia za kuguswa na kifo cha Golden Jacob 'KingZilla', hiyo imekuwa tofauti kwa mkongwe Juma Nature 'Kiroboto'.

Nature aliyewahi kutamba na ngoma kama Hakuna kulala na Sonia, yeye amemuaga Zilla kitofauti baada ya kuachia nyimbo ambayo ina ujumbe wa kumuaga msanii huyo.

Ukaribu wa wasanii hawa ulianzia pale Zilla alipomuomba Nature kufanya marudio ya wimbo wa Sonia (Remix) na kibao hiko nacho kilitamba vile vile kutokana na aina ya miondoko ya mistari ya mashairi iliyotumika katika ngoma hiyo.

Katika wimbo huu wa mwisho wa Nature alioandika maalum kwa marehemu Zilla, alisikika akiimba zaidi kwa sauti ya manung'uniko huku mstari wake wa mwisho akimalizia kwa kusema "Resting in peace my blood".

Kumekuwa na kawaida kwa wasanii kuingia studio na kufanya wimbo pale msanii mwenzao anapotangulia mbele za haki, hiyo imetokea awali baada ya Mangwair kufariki, wasanii Nikki Mbishi, Babuu wa Kitaa, Cliff Mitindo walitunga wimbo 'Moment of Silence' wakielezea namna walivyokuwa wameguswa na kifo Albert Mangwair.