Mo Dewji aibuka, aamsha shangwe Uwanja Taifa

Muktasari:

Mwekezaji wa Klabu ya Simba, Mohammed Dewji ‘Mo’ leo Jumatano kwa mara ya kwanza amehudhuria Uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam kushuhudia mechi kati ya timu hiyo na Mbambane Swallows ya Swaziland.

Dar es Salaam. Mashabiki wa Simba wamelipuka kwa shangwe baada mwekezaji za klabu hiyo, Mohammed Dewji ‘Mo’ kuonekana kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Taifa, leo Jumatano Novemba 28, 2018.

Mo ametinga Taifa kuwashuhudia Simba ikicheza mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Mbambane Swallows ya Swaziland.

Kuonekana kwa bilionea huyo kijana barani Afrika uwanjani hapo, kumeibua shangwe kwa mashabiki wa mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara ambao mara kadhaa wamekuwa wakimshangilia.

Mara baada ya kuwasili alisalimia mashabiki nakuamsha hoihoi huku wakiimba MO... MO... MO.

Kabla ya kushuka pamoja na mgeni rasmi kwenye kipute hicho, mbunge wa Ilala (CCM), Mussa Zungu kwenda kuzisalimia timu hizo na wakati wanatoka uwanjani kwenda kukaa jukwaani, aliwapungia mikono jambo lililozidisha shangwe kwa mashabiki hao wa Klabu ya Simba.

Mwekezaji huyo, alitekwa alfajiri ya Oktoba 11, 2018 katika hoteli ya Colosseum iliyopo Oysterbay jijini Dar es salaam na usiku wa kuamkia Oktoba 20, 2018 alitelekezwa kando ya viwanja vya vya Gymkhana jijini humo.