Zidane kijasho chamtoka kisa Hazard kuumia

Muktasari:

Hazard, 28, alikuwa kwenye kiwango bora kabisa katika mchezo wa sare ya 2-2 dhidi ya PSG uwanjani Santiago Bernabeu kabla ya nafasi yake kuingizwa Gareth Bale dakika ya 70 baada ya kuumia. Na Zidane amekuwa mwenye hofu kutokana na majeruhi ya mchezaji wake huyo.

LONDON, ENGLAND . ZINEDINE Zidane amekiri kuwa na wasiwasi juu ya hali ya supastaa wake Eden Hazard kama atakuwa fiti kukipiga kwenye El Clasico mwezi ujao.
Supastaa huyo wa Real Madrid, Hazard aliumia enka kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Paris Saint-Germain uliopigwa juzi Jumanne usiku.
Kutokana na hilo, Hazard anaweza kuwa nje ya uwanja kwa wiki kadhaa na kumtia wasiwasi kocha Zidane kama atakuwa fiti kwenda kuwakabili mahasimu wao Barcelona huko Nou Camp, Desemba 18.
Hazard, 28, alikuwa kwenye kiwango bora kabisa katika mchezo wa sare ya 2-2 dhidi ya PSG uwanjani Santiago Bernabeu kabla ya nafasi yake kuingizwa Gareth Bale dakika ya 70 baada ya kuumia. Na Zidane amekuwa mwenye hofu kutokana na majeruhi ya mchezaji wake huyo.
“Nina wasiwasi kuhusu Hazard. Alionekana kuwa kwenye maumivu makali kuliko hata ilivyoonekana awali. Aliumia enka, matumaini ni kwamba sio maumivu makubwa ya kumfanya akosekane uwanjani kwa muda mrefu. Tutafahamu ukubwa wa jambo hilo baada ya kufanyiwa vipimo,” alisema Zidane.
Hazard alinaswa na Los Blancos kutoka Chelsea kwenye dirisha lililopita la majira ya kiangazi kwa ada inayoweza kupanda hadi kufikia Pauni 150 milioni. Na tangu atue kwenye kikosi hicho amecheza mechi saba na kufunga bao moja. Hazard akikosa El Clasico basi anaweza kuzikosa pia Alaves, Espanyol, Club Brugge na Valencia.