Yanga yapewa mbinu za kuifunga Zesco

Muktasari:

Yanahesabika masaa Yanga kushuka dimbani kucheza na Zesco ya Zambia, mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, beki wa zamani wa timu hiyo, amewapa mbinu za kuwafunga wapinzani wao.

YANGA inashuka dimbani saa 10:00 jioni kumenyana na Zesco, mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo beki wa zamani wa timu hiyo Abdallah Shaibu 'Ninja' amewapa neno Wanajangwani kuelekea mchezo huo.
Ninja ambaye kwa sasa anacheza LA Galaxy ya Marekani, amewataka mastaa wa Yanga kujiamini na kuhakikisha wanautumia vyema uwanja wa taifa kupata matokeo ili ugenini wakapiganie sare.
Akisisitiza kwamba wachezaji wa Yanga wakijiamini itakuwa rahisi kwao kucheza bila presha na wakapata matokeo ya kuwafanya wasonge mbele zaidi kwenye michuano hiyo.
"Yanga ina wachezaji wanaoweza kuamua matokeo, wasiangalie Zesco wana rekodi gani bali wao waingie wakitaka kuweka rekodi dhidi yao,naamini wakifanya hivyo watafanya maajabu"
"Pia wasiingie kwa kuwabeza Zesco kisa wapo nyumbani kwani nao wamekuja kupambana kuhakikisha wanapata nafasi ya kusonga mbele kwenye michuano hiyo"
"Mashabiki wana nafasi kubwa ya kuwaunga mkono wachezaji, hivyo nao wajitokeze kwa wingi kuwapa moyo ili waone hawapo pekee yao"amesema.