Walker kupangua ukuta wa England

Muktasari:

  • Walker aling’ara katika fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika Russia mwaka huu, licha ya kuchezwa katika nafasi isiyo yake ya mlinzi wa pembeni kushoto badala ya kulia alikozoea lakini alicheza kwa umahiri mkubwa.

London, England. Kocha wa England, Gareth Southgate ameweka bayana lengo lake ni kubadili namba ya beki wa Manchester City, Kyle Walker katika kikosi chake.

Walker aling’ara katika fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika Russia mwaka huu, licha ya kuchezwa katika nafasi isiyo yake ya mlinzi wa pembeni kushoto badala ya kulia alikozoea lakini alicheza kwa umahiri mkubwa.

Kocha wa England, Southgate amemwambia mlinzi huyo asiwe na wasiwasi wa kukosa namba kwani sasa anafikiria kumtumia kama mlinzi wa kati, kutokana na kujituma kwake pamoja na umakini alionao uwanjani.

“Kutokana na tatizo lililojitokeza katika mechi za hivi karibuni nimepanga kuanza kumtumia Walker kama mlinzi wa kati badala ya kucheza pembeni, tuna tatizo katika eneo hilo,” alisema Southgate.

Kocha huyo alifichua kuwa mbali ya mlinzi huyo pia atajaribu kuwachezesha katika nafasi hiyo, Joe Gomez, Kieran Trippier na chipukizi anayeichezea Liverpool mwenye miaka 19, Trent Alexander-Arnold.

Walker ambaye majeruhi yamemfanya awe nje ya kikosi cha sasa cha England akiikosa michezo ya hivi karibuni alisema atahakikisha anarejesha namba yake.

Mchezaji huyo hayupo kwenye kikosi cha England kitakachoshuka dimbani leo hii mjini Leicester kucheza na Uswisi katika mchezo wa kirafiki.