Scholes aukubali muziki wa Fernandes

Muktasari:

Kiungo huyo, alijiunga na Manchester United akitokea Sporting Lisbon siku chache kabla ya dirisha la usajili la Januari kufungwa kwa ada ya uhamisho wa Pauni 68 million.

London, England .KIWANGO alichokionyesha kiungo mpya wa Manchester United,  Bruno Fernandes katika mchezo wa Europa Ligi  dhidi ya  Club Brugge kwenye uwanja wa Old Trafford, kimemkuna Paul Scholes.
Fernandez aliiongoza Manchester United kuibuka na ushindi wa mabao 5-0 katika mchezo huo wa raundi ya 32 ya Europa Ligi baada ya mchezo wa kwanza kutoka sare ya bao 1-1 nchini Ubelgiji.
Scholes alisema,"Ameifanya timu kuvutia katika kushambulia, maisha yamekuwa mepesi. Unaweza kujiuliza ingekuwaje kama Manchester United ingeamua kumsajili tangu mwanzoni mwa msimu."
Tangu amejiunga na klabu yake hiyo, Fernandez amekuwa mchezaji muhimu kutokana na uwezo aliouonyesha wa kutengeneza na kufunga mabao katika michezo mbalimbali aliyocheza.
Scholes ambaye alikuwa akichambua katika kituo cha BT Sports akiwa na Owen Hargreaves, walionekana kuvutiwa na kiwango cha nyota huyo wa Kireno ambaye tangu atue  Old Trafford hawajapoteza mchezo hata mmoja kati ya saba.
Upande wake Hargreaves alisema "Ujio wake umerahisisha mambo hata ukiwaangalia wachezaji wenzake kila baada ya michezo kumalizika wamekuwa na tabasamu usoni, mashabiki wameanza kuliimba jina lake,"
Ighalo, ambaye naye alisajiliwa pamoja na Fernandez dirisha lililopita la usajili akitokea China, alipachika bao lake la kwanza akiwa na mashetani hao wekundu wa Old Trafford.
Mbali na Fernandez na Ighalo waliofunga bao moja kila mmoja, mabao mengine ya Manchester United katika mchezo huo, yalifungwa na McTominay na Fred aliyefunga mara mbili.