Pato:Thamani yangu inarejea

Muktasari:

Beki wa Polisi Tanzania, Pato Ngonyani ni kati ya wachezaji ambao wanaonyesha kiwango cha juu kwenye ligi kuu Bara,jambo alilosema ana kitu anakilenga kwa ajili ya maendeleo ya kazi yake.

BEKI wa Polisi Tanzania, Pato Ngonyani amesema ubora wa kiwango chake unatokana na namna anavyoisaidia timu yake kwenye mechi ngumu, jambo analoliamini linarejesha thamani yake.

Pato alijiunga na Polisi Tanzania akitokea African Lyon ambako alipelekwa kwa mkopo na Yanga, amesema msimu huu anautazama kama wa kumpa mafanikio kwenye kazi zake.

Amesisitiza kwamba thamani ya kazi yake inatokana na uwezo wa kuisaidia timu kipindi ambacho inalemewa, akiamini kupitia hilo msimu ujao atakuwa na hatua nyingine ya maendeleo.

"Unajua mchezaji anapoondoka Simba na Yanga wengi wanaamini kwamba kiwango chake kimekwisha, ili kuondoa mawazo yao potofu lazima wachezaji tudhihirishe uwanjani."
"Binafsi kuondoka Yanga nilichukulia kama ni moja ya changamoto za kazi natakiwa kuonyesha uwezo na sio kulalamika, mchezaji anapaswa kucheza popote ili mladi tu kazi yake iwe na thamani ndipo anaweza akafaidika nayo,"anasema.