Mzamiru arudi kupigania namba

Muktasari:

Mzamiru ambaye mchezo wake wa mwisho kuitumikia simba ulikuwa ni dhidi ya Yanga jana kaanza mazoezi mepesi pamoja na kikosi chake tayari kwaajili ya kuongeza nguvu kikosini humo.

BAADA ya kukaa nje kwa muda wa wiki sita kiungo wa Simba, Mzamiru Yassin amesema ana kazi kubwa kuhakikisha anarudi kikosini na kuipambania timu yake kutetea taji wanaloshikilia.

Mzamiru alikuwa anasumbuliwa na goti alisema ameanza mazoezi mepesi na kikosi chake huku akihofia namba yake kikosini kutokana na wachezaji waliopo kufanya vizuri.

"Sio kazi rahisi kurudi kikosini ukiwa umetoka majeruhi na uliowaacha wakiwa hawana cha kupoteza mara baada ya kupewa nafasi hivyo ni jukumu langu kupambana zaidi ili niweze kumshawishi mwalimu aweze kuniamini tena," alisema.

Alisema anafurahia kuona timu yake inapata matokeo huku akiweka wazi kuwa ubingwa upo miguuni mwa wachezaji wakiendelea kupambana zaidi wana kila sababu ya kutete ubingwa na kuendeleza mazuri waliyoyaonyesha mashindano ya kimataifa.

"Kwa namna timu ilivyo kwenye ari ya ushindani nina kila sababu ya kuweka wazi kuwa hakuna timu ambayo inaweza kutupoka labda sisi wenyewe wachezaji tuamue kuuachia kwani majukumu yote yapo chini yetu," alisema.