Mudathiri atoa onyo Azam

Muktasari:

Mudathir Yahya alinaswa na Azam FC mwaka 2012 baada ya kutamba katika mashindano ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 ya Copa Coca Cola ambayo aliichezea timu ya Mkoa wa Mjini Magharibi.

SIKU moja baada ya kuwasili Jijini Dar es salaam, kiungo wa Azam FC,  Mudathir Yahya amesema kuwa yupo fiti kuelekea mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mbao FC .

Mudathiri amesema kuwa wakati ligi iliposimamishwa yeye na wachezaji wenzake walikuwa wanapewa muongozo kutoka kwa kocha juu ya mazoezi gani wafanye.

" Nipo sawa kwa kuwa, wakati ligi imesimama kocha alikuwa anatupa utaratibu juu ya mazoezi ambayo tulitakiwa kuyafanya.

" Unajua mchezaji wa mpira akikaa muda mrefu bila ya kucheza mechi, kiwango chake huwa kinashuka, hivyo mimi nafikiri suala hili, halijaathiri mchezaji mmoja ni karibia wote, lakini tunafanya mazoezi kwa juhudi kuhakikisha nakuwa sawa ili kurudi kwenye hali yangu" amesema Yahya

Aidha Mudathir alieleza sababu iliyomfanya achelewe kujiunga na timu Kwa siku tano tokea ianze mazoezi.

" Nilikuwa nauguliwa na wazazi wangu upande wa baba na mama, yaani bibi na babu yangu wote wanaumwa, babu yeye amefanyiwa upasuaji na bibi anaumwa, halafu hawajiwezi kwa lolote, hivyo ilinibidi kuwahudumia kwa siku kadhaa ndio maana nikachelewa" alisema kiungo huyo.