Messi amtumia ujumbe Neymar

Muktasari:

Kwa msimu wa pili mfululizo, Barcelona ilikwenda kucheza mechi za marudiano za hatua ya nusu fainali ikiwa na mtaji mzuri wa mabao kwenye ushindi wa kwanza, lakini mara zote waliteseka na kutupwa nje, ikiwamo lile tukio la msimu ulipita lililotokea Anfield walipopigwa 4-0 kwenye mechi ya marudiano wakati ile ya kwanza ya Nou Camp walishinda 3-0.

BARCELONA, HISPANIA . NDO hivyo. Lionel Messi amemwomba Neymar arudi kukipiga Barcelona baada ya kuumizwa na namna walivyotupwa nje kwa udhalilishaji mkubwa kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya na Liverpool msimu uliopita.
Kwa msimu wa pili mfululizo, Barcelona ilikwenda kucheza mechi za marudiano za hatua ya nusu fainali ikiwa na mtaji mzuri wa mabao kwenye ushindi wa kwanza, lakini mara zote waliteseka na kutupwa nje, ikiwamo lile tukio la msimu ulipita lililotokea Anfield walipopigwa 4-0 kwenye mechi ya marudiano wakati ile ya kwanza ya Nou Camp walishinda 3-0.
Kwa mujibu wa France Football, baada ya kutolewa kwa udhalilishaji, nahodha wa Barca alichukua simu yake na kumtumia meseji ya WhatsApp staa Neymar akimwambia: “Tukiwa pamoja tu ndio tunaweza kushinda Ligi ya Mabingwa Ulaya. Nakutaka urudi. Miaka miwili ijayo, nitaondoka na utabaki wewe, utachukua nafasi yangu.”
Mkurugenzi wa soka wa Barcelona, Eric Abidal amethibitisha kwamba suala la kumrudisha supastaa huyo wa Kibrazili kwenye kikosi chao ni jambo lililopo kwenye mpango. Neymar alionekana kuwa kwenye nafasi ya kurudi Barcelona kwenye dirisha lililopita la uhamisho wa majira ya kiangazi, lakini alibaki PSG huku ikidaiwa kwamba kuna uwezekano mkubwa dili hilo likakamilishwa kwenye usajili ujao wa majira ya kiangazi huko Ulaya.
Baada ya kusajiliwa kwa ada iliyovunja rekodi ya dunia ya Pauni 198 milioni mwaka 2017, Neymar ameshindwa kuendana na kasi huku akiandamwa na majeruhi mfululizo yanayomtibulia kwenye jitihada zake za kubeba tuzo ya Ballon d’Or. Real Madrid nao waliingia kwenye vita ya kumtaka Neymar.