Mbappe kuivuruga Real Madrid

Muktasari:


Zinedine Zidane ameonyesha mahaba yake ya wazi kwa staa wa PSG, Kylian Mbappe huku Rais wa Real Madrid, Florentino Perez akiwaza kumfanya kinda huyo kuwa mfalme mpya wa Santiago Bernabeu.

Madrid, Hispania .KOCHA wa Real Madrid, Zinedine Zidane na jeshi lake wanawaza njia za kutumia ili kumdhibiti mshambuliaji matata wa Paris Saint German, Kylian Mbappe.
Hata hivyo, kwa upande mwingine Zinade na mabosi zake kwa nyakati tofauti watakuwa wakimuangalia Mbappe akifanya yao uwanjani kisha kufanya maamuzi magumu ya kuvunja benki na kupata huduma yake.
Kwa upande wake, supastaa mpya wa Real Madrid, Eden Hazard amefichua kuwa Mbappe ni mchezaji mzuri na kiwango chake kimekuwa kikiimarika kila kukicha na kwamba, yuko tayari kusaidia kumleta Santiago Bernabeu.
Real Madrid baadaye usiku itaikaribisha PSG kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu huku macho yakiwa kwa Mbappe.
Licha ya uwepo wa Neymar Jr, Mauro Icard na Di Maria kwenye kikosi cha PSG, lakini tahadhari kubwa imewekwa kwa Mbappe kutokana na kasi yake katika kufumania nyavu.
Katika mchezo wa kwanza uliofanyika jijini Paris, Ufaransa Real Madrid ilichapwa mabao 3-0 kisha ikalazimisha sare na Club Brugge na kupata ushindi.  
PSG inaingia kwenye mchezo huo ikiwa tayari imeshatinga hatua ya 16 bora, ikishinda mechi nne dhidi ya Madrid, Galatasaray na Brugge na kuvuna alama 12 ikiwa kileleni mwa msimamo.