Kichuya, Okwi wakabidhiwa silaha za Waarabu Simba

Muktasari:

Simba imefanya mazoezi hayo ikiwa na kikosi cha nyota wote 18,  ambao walisafiri na timu kutoka Kisiwani Zanzibar walikokuwa na michuano ya Kombe la Mapinduzi kuja Dar es Salaam. Zanzibar imebaki Simba B ikiendelea na mashindano hayo.

Dar es Salaam. Kocha wa Simba, Patrick Aussems amejipanga kutumia mbinu ya kushambulia kutokea pembeni katika mchezo wao dhidi ya JS Saoura ya Algeria utakaopigwa Jumamosi hii Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Katika mazoezi ya Simba yaliyofanyika Uwanja wa Boko Veterani, kocha huyo alikuwa aliwaelekeza wachezaji wake kupiga pasi chache fupi katikati mwa kiwanja na kisha viungo hao kupiga pasi ndefu pembezoni mwa uwanja kwa mawinga au mabeki wa pembeni.
Mabeki hao jukumu lao lilikuwa ni kupiga krosi kwenye eneo la hatari la timu pinzani na kuwaachia washambuliaji kama Emmanuel Okwi,,Shiza Kichuya na wengine kumaliza kazi.
Mwanzo Aussems aliwaelekeza kupiga krosi za juu na baadaye alibadilisha wakawa wanapiga za chini kwa mtindo wa kuzirudisha nje ya eneo la hatari la wapinzani.
Kocha huyo aliwataka wachezaji hao wa Simba kutopiga idadi kubwa ya pasi kuelekea langoni mwa wapinzani na badala yake alitaka ziwe tano tu ukijumlisha na krosi ya mwisho.
Katika mazoezi hayo mshambuliaji Emmanuel Okwi raia wa Uganda na kiungo Mzambia Cletous Chama walikuwa kivutio kutokana na ustadi wao wa kumalizia mipira ya krosi.