Maguli amkosha kocha wake

Muktasari:

Maguli anasifika kwa uwezo wake wa kutumia nguvu na kuwapita mabeki wa timu pinzani na kufunga magoli.

KOCHA wa timu ya FC Platinums, Pieter De Jongh ameonyesha kukubali kiwango cha mshambuliaji wa Kitanzania, Elius Maguli anayeichezea timu hiyo ya Zimbabwe.

Maguli ambaye amejiunga na klabu hiyo wakati wa dirisha dogo akitokea Nakambala Leopards ya nchini Zambia ameonyesha uwezo mkubwa tangu ajiunge na timu hiyo.

Pieter amesema mchezaji huyo ana uwezo mkubwa wa kumiliki mpira na kufunga kitu ambacho amekionyesha mara kwa mara.

"Maguli sio mchezaji mdogo ni mchezaji mkubwa, anatambua kile ambacho anakifanya, mazoezini amekuwa akifanya makubwa na anafunga," alisema.

Kocha huyo alisema katika kikosi chake kuna washambuliaji watatu hatari, Maguli ni mmojawapo.

Licha ya sifa zote hizo Maguli amecheza mchezo mmoja tu huku janga la ugonjwa wa virusi vya corona likatibua mambo na kufanya ligi isimame.

Maguli akiwa Nakambala Leopards aliifungia timu hiyo magoli matano na baadaye alivunja mkataba wake na kutimkia FC Platinums.