Liverpool kuendeleza ubabe

Muktasari:

Liverpool wanahitaji ushindi ili kuzidi kujiweka katika sehemu nzuri katika usukani wa Ligi Kuu nchini Uingereza.

KESHO Jumamosi Ligi Kuu ya Uingereza inaendelea huku Liverpool wakiwa kibaruani dhidi ya Brighton kuhakikisha wanapata ushindi ili kuendelea kukaa kileleni, mechi hiyo itapigwa Uwanja wa Anfield.

Liverpool wanaongoza ligi wakiwa na pointi 37, kwenye mechi hiyo itakayochezwa saa 12 jioni wanahitaji ushindi  ili kuendelea kujiimarisha kileleni ambapo Leicester City ambaye anashika nafasi ya pili ana pointi 29 huku wote wakicheza mechi 13.

Mchezo mwingine mkali ni wa Manchester City dhidi ya Newcastle utakaochezwa saa 9.30 alasiri huu nao utakuwa mkali kama City watashinda watasogea nafasi ya pili.

Mpaka hivi sasa Man City wanashika nafasi ya tatu wakiwa na pointi 28 huku Leicester City wanaoshika nafasi ya pili wakiwa na pointi 29.

Man City wanatakiwa kupata ushindi wakiwa ugenini Uwanja wa St James Park ili kuzidi kusogea juu zaidi.

Michezo mingine itakayopigwa ni baina ya Burney na Crystal Palace, Chelesea dhidi ya  West Ham, Tottenham na Bournemouth wakati a Southampton watacheza dhidi ya Watford yote ikichezwa kesho Jumamosi.