Kwa Snura kuna majanga

Muktasari:

Huko kwenye mitandao ya kijamii, watu wamekuwa wakitokwa povu wakimtaka Snura kuachana na Minu kwa kuwa wana tofauti kubwa ya umri.

HAPA kwa Snura kweli kuna majanga unaambiwa, lakini mwenyewe wala hana habari ndio kwanza anakoleza malovee. Iko hivi staa huyo wa Bongo Flava anayesumbua kwenye miondoko ya kishua, Snura Mushi a.k.a mama Majanga amesema anafurahia penzi lake na Minu na hajali wakimuita mtu wake huyo Serengeti Boys.

Snura, ambaye anatamba na ngoma ya Najidabua, amesema maneno yanayosemwa kwenye mitandao ya kijamii anayaona sana, lakini hayawezi kumrudisha nyuma wala kumfanya asifurahie penzi lake kwa Minu.

Huko kwenye mitandao ya kijamii, watu wamekuwa wakitokwa povu wakimtaka Snura kuachana na Minu kwa kuwa wana tofauti kubwa ya umri.

Mwanaspoti lilichonga naye na mwenyewe akafunguka, katika maisha kila mtu ana staili yake kuishi kutokana na mazingira aliyopo hivyo, kama watu wanamwona amebadilika kwa sasa, basi wajue Minu ndio kila kitu.

“Hii hakuna hata kupindisha, hayo maswali ya wanitumie niwajibu tu na huyo wanayemuita Serengeti Boy ndio amesababisha niwe hivi na hii yote ni kutokana na kupata mapenzi ya dhati. Kwa kifupi mioyo yetu inaendana.

“Halafu unajua vitu vingine vinanishangaza sana, watu hao hao wananichambaa mitandaoni na hao hao wanataka uweke siri mambo yako.”