Klopp agoma kumpasua Salah

Muktasari:

Kocha Jurgen Klopp alisema maumivu hayo yalikuja kuongezeka zaidi baada ya kuchezewa rafu na kiungo wa Manchester City, Fernandinho na hilo linamfanya ashindwe kupona kwa haraka.

LIVERPOOL, ENGLAND . LIVERPOOL imefuta mpango wa kumfanyia upasuaji mshambuliaji wao Mohamed Salah licha ya kuwapo na hofu kubwa ya majeruhi ya enka yasiyotaka kupona.
Staa huyo amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya enka kwa wiki sita mfululizo tangu alipochezewa rafu na mchezaji wa Leicester City, Hamza Choudhury mapema mwezi uliopita.
Salah amekuwa akifanya mazoezini huku na tatizo hilo la maumivu na amekuwa akipatiwa matibabu siku chache kabla ya kila mechi anayoingia kucheza.
Kocha Jurgen Klopp alisema maumivu hayo yalikuja kuongezeka zaidi baada ya kuchezewa rafu na kiungo wa Manchester City, Fernandinho na hilo linamfanya ashindwe kupona kwa haraka.
Alipoulizwa kama mchezaji huyo anahitaji kufanyiwa upasuaji, Klopp alisema: “Hapana. Aliumia kwenye mechi ya Leicester City, akapona kisha akaumia tena kwenye mechi ya Man City.
“Sio kitu siriazi sana, hivyo tutamwaacha kwa siku chache za kupumzika na kisha tunamtumia. Lakini, tutakuwa tunatazama kama anafanya mazoezi kiasi cha kutosha na kama atakuwa tayari kucheza.”