Kilimanjaro Queens yaipigia hesabu Uganda

Muktasari:

Mwaka jana Kilimanjaro Queens ilitwaa ubingwa mbele ya Uganda baada kuizidi uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa ingawa zote zilimaliza zikiwa na pointi saba.

KOCHA mkuu wa timu ya taifa ya wanawake ya Tanzania Bara 'Kilimanjaro Queens', Bakari Shime ametabiri ugumu wa mechi ya nusu fainali ya mashindano ya Afrika Mashariki kesho Jumamosi dhidi ya Uganda huku akipanga kuchanga upya karata zake kimbinu.

Mechi hiyo ambayo itakuwa ya pili  kuanzia saa 10 jioni baada ya nusu fainali ya kwanza baina ya Kenya na Burundi itakayochezwa saa 7.45 mchana.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jijini leo Ijumaa, Shime alisema kuwa amewatazama vizuri Uganda na amejipanga kukabiliana nao.

"Uganda ni timu nzuri na tunaamini mechi itakuwa ngumu lakini kwa upande wetu tumejiandaa kikamilifu kuhakikisha tunapata ushindi.

"Tuliwakosa wachezaji wetu Julitha Aminiel na Asha Bilali kwenye mchezo uliopita kutokana na kutumikia adhabu ya kadi na tunatarajia watakuwepo mchezo ujao na pia atakuwepo mchezaji bora wa mashindano ya Cosafa, Eneckia Kasonga ambaye  alikuwa anamalizia mitihani yake," alisema Shime.

Kocha huyo alisema kuwa atabadili baadhi ya mbinu zake dhidi ya Uganda tofauti na mechi zilizopita kutokana na namna alivyowaona katika mechi zao