'Jirani' wa RC Mtaka, Simiyu avuna mamilioni ya M-bet

Muktasari:

Mkuu wa Kitengo cha Kodi za Kubahatisha Mamlaka ya Mapato (TRA) Mkoa wa Ilala, Shabani Rashid Mwanga amesema unaposhinda kiasi chochote, serikali inapata kodi yake moja kwa moja na kuongezea fedha za kufanyia maendeleo nchini.

Dar es Salaam. Ukisikia zari la mwaka 2019, basi ni hili alilokutana nalo, Golesu Maduhu (23) mkazi wa Bariadi, mkoani Simiyu, jirani na yalipo Makao Makuu ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, ambaye ameibuka na kitita cha Sh 56,137,550 baada ya kubahatisha kwa usahihi mchezo wa Perfect 12, unaoendeshwa na Kampuni ya M-Bet Tanzania.
Maduhu ameweza kubahatisha matokeo ya droo ya mwezi Desemba mwaka jana na kuwa mshindi wa kwanza kuzawadiwa fedha kutoka Kampuni ya M-Bet kwa mwaka huu baada ya kupatia kiusahihi michezo yote 17.
Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa fedha zake, Maduhu alisema kuwa amefurahi kupata kiasi hicho cha fedha ambacho kitamsaidia katika maisha yake.
Maduhu amesema kuwa ametumia Sh 1,000 kupata mamilioni hayo ya fedha na kuwaomba Watanzania kujiunga na michezo ya Kampuni ya M-BET ambayo inachangia kubadili maisha.
Meneja Masoko wa Kampuni ya M-Bet Tanzania, Allen Mushi alisema kuwa katika fedha hizo, Serikali imepata Sh. 11.2 mil
ikiwa ni kodi ya ushindi.
“Nawaomba Watanzania washiriki katika michezo ya kubahatisha ya M-bet ambayo mwaka 2018, iliwazawadia jumla ya washindi 20 ambao walipata mamilioni ya fedha na kubadili maisha yao,” alisema Mushi.
Mkuu wa Kitengo cha Kodi za Kubahatisha Mamlaka ya Mapato (TRA) Mkoa wa Ilala, Shabani Rashid Mwanga naye aliwaomba Watanzania kushiriki katika michezo hiyo ili kuchangia maendeleo ya nchi.
Mwanga alisema kuwa unaposhinda kiasi chochote, serikali inapata kodi yake moja kwa moja na kuongezea fedha za kufanyia maendeleo nchini.
“Naishukuru M-Bet ambayo kila mara imekuwa ikitoa washindi wamekuwa wakipata mamilioni ya fedha na kuchangia pato la taifa, ni chanzo kizuri sana cha mapato kwa ajili ya maendeleo nchini,” alisema Mwanga.
Meneja wa Leseni na Huduma za Sheria wa Bodi ya Michezo ya kubahatisha nchini, Catherine Lamwai aliipongeza Kampuni ya M-bet kwa kuweka kuendelea kupata washindi wengi na kujizolea mamilioni ya fedha.
“Bodi ya Michezo ya Kubahatisha imekuwa ikifuatilia na kusimamia michezo ya kubahatisha kutokana na kupata washindi wengi.
Wametufurahisha sana kutokana kuchangia pato la taifa kupitia mchezo wa Perfect 12,” alisema Lamwai.