Churchill akumbuka wacheshi wote buda

Muktasari:

Tumenzisha tuzo ziitwazwo Taji Recoginition Awards’ kutambua michango mbalimbali ya wabunifu wa ucheshi kwenye tasnia hii. Mwaka huu tumefanya kuchagua sisi ila kuanzia mwaka ujao, itakuwa ni shughuli ya mashabiki kuamua nani anayestahili kutuzwa”

MVUNJA mbavu lejendari Daniel Ndambuki mwasisi wa kipindi maarufu ya Stand Up Comedy nchini, Churchill na vilevile ‘International Africa Laugh Festival’ kazindua tuzo za kuwaenzi wacheshi hapa nchini.
Makala ya kwanza ya tuzo hizo zitakazokuwa zikifahamika kama Taji Recognition Awards, zilifanyika usiku wa Ijumaa katika ukumbi wa KICC, Nairobi.
Ilikuwa ni kwenye makala ya tatu ya Stand Up Comedy International Africa Laugh Festivals ambayo huwashusha wacheshi shoka kutoka kila upande wa bara hili mjini Nairobi ili kuonyesha uwezo wao.
Baada ya wavunja mbavu zaidi ya wanane kupanda jukwani na kuwaacha mashabiki hoi, Churchill ambaye pia ni mwasisi wa Laugh Festival, alifunga shoo kwa kutangaza ujio wa tuzo  hizo alizosema zitafanyika kila mwaka kutambua michango ya wadau waliotoa mchango mkubwa wa ucheshi kwenye tasnia.
Tumenzisha tuzo ziitwazwo Taji Recoginition Awards’ kutambua michango mbalimbali ya wabunifu wa ucheshi kwenye tasnia hii. Mwaka huu tumefanya kuchagua sisi ila kuanzia mwaka ujao, itakuwa ni shughuli ya mashabiki kuamua nani anayestahili kutuzwa”
Kwenye makala ya kwanza ya tuzo hizo, mcheshi Njugush alituzwa kwa ubunifu wake wa vichekesho vya mitandaoni ambao umemfanya kuwa maarufu na kuvutia utazamaji mkubwa sana kwenye YouTube, Instagram na Facebook.
Tuzo nyingine ilimwendea mwanahabari Emmanuel Juma kwa kitengo chake cha ucheshi kwenye runinga ya NTV ‘Bulls Eye’ ambapo yeye hukusanya matukio ya siasa yanayotokea nchini kila wiki na kisha kuyawasilisha Ijumaa kwa njia ya ucheshi.