Aussems aweka mziki mnene kuivaa Ruvu Shooting

Muktasari:

Aussems anahitaji ushindi katika mchezo huu ili kuweka utulivu kwa mashabiki wa Simba.

KOCHA wa Simba, Patrick Aussems amepanga kikosi kikali katika mchezo wao dhidi ya Ruvu Shooting utakaopigwa leo Jumamosi kuanzia saa 10 jioni uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Katika kikosi hicho, amewapanga Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohamed Hussein 'Tshabalala', Tairone Santos, Pascal Wawa, Gerson Fraga, Hassan Dilunga, Mzamiru Yassin, Meddie Kagere, Miraj Athuman na Francis Kahata.
Aussems amefanya mabadiliko eneo la kiungo baada ya kumuanzisha Hassan Dilunga na kumuondoa Jonas Mkude huku akiwaacha Gerson Fraga na Mzamiru Yassin.
Mabadiliko mengine ambayo ameyafanya ni kumuanzisha Miraj Athuman eneo la ushambuliaji na kumuondoa Ibrahim Ajib ambaye alikuwa anaanza michezo ya hivi karibuni.
Mchezo huu unatajwa kuwa wa mwisho kwa Aussems baada ya kudaiwa kwamba tayari amefanya mazungumzo na moja ya timu nchini Afrika Kusini na kilichobaki ni kuangalia tu hatma yake ndani ya Simba baada ya kuondoka nchini bila ruhusa kutoka kwa viongozi wake mapema wiki hii.