Messi kumchunia CR7 kura Ballon d’Or

PARIS, UFARANSA. SUPASTAA, Lionel Messi hatampigia kura mpinzani wake wa jadi Cristiano Ronaldo kwenye tuzo za Ballon d’Or.

Muargentina huyo aliyejiunga na Paris Saint-Germain baada ya kuachana na Barcelona dirisha lililopita la uhamisho wa majira ya kiangazi, ameshinda tuzo hiyo mara sita, moja zaidi ya mpinzani wake, Ronaldo, ambaye msimu huu anakipiga huku Manchester United baada ya kuondoka Juventus.

Ronaldo na Messi wote wamejumuishwa kwenye orodha ya mastaa 30 wanaochuana kuwania tuzo hiyo ya Ballon d’Or 2021.

Messi ameweka wazi, hatampigia kura mkali huyo wa zamani wa Real Madrid, badala yake kura zake zitakwenda kwa mastaa wawili anaocheza nao pamoja huko PSG kwa sasa, akidai kwenye kura zake tatu, mbili zitawahusu Kylian Mbappe na Neymar.

Na moja iliyobaki, anaweza kumpigia ama straika wa Bayern Munich, Robert Lewandowski au wa Madrid, Karim Benzema.

Messi aliambia LíEquipe: “Ni wazi kabisa, kuna wachezaji wawili kwenye timu yangu nitakaowapigia kura, Ney na Kylian.

“Baada ya hapo, kutakuwa na wachezaji ambao nitaangalia uwezo wao wa msimu, kama Lewandowski, Benzema. Siku hizi, uzito umewekwa kwenye mataji zaidi, ukishinda Ligi ya Mabingwa Ulaya, Euro na Copa America.”