Kina Messi kuliamsha na Brugge

London, England. Baada ya mechi za jana za Ligi ya Mabingwa Ulaya, kipute hicho kinaendelea leo kwa mechi kadhaa kuchezwa.Mshambuliaji mpya wa Paris Saint-Germain, Lionel Messi kwa mara ya kwanza ataonekana kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa ndani ya jezi isiyokuwa ya Barcelona, wakati timu yake itakapokwenda ugenini kucheza na Club Brugge.PSG imepangwa kundi A, huku mashabiki wakisubiri kuona kile  itakachofanya kwenye michuano hiyo kwa kuwa na kikosi chenye safu hatari ya ushambuliaji inayoundwa pia na wakali Kylian Mbappe na Neymar.Mechi nyingine kwenye kundi hilo linalotajwa kuwa ni la kifo, itakutanisha chama la Pep Guardiola, Manchester City lenye wachezaji wakali kama Kevin De Bruyne, Jack Grealish, Raheem Sterling kwa kuwatazama kwa uchache na Wajerumani RB Leipzig.Katika kundi B, mabingwa wa Hispania, Atletico Madrid ambao safu yao ya ushambuliaji itakuwa na Luis Suarez na Antoine Griezmann itakuwa nyumbani Wanda Metropolitano kucheza na FC Porto, wakati kocha Jurgen Klopp na wakali wake Mohamed Salah na Sadio Mane watakuwa Anfield wakati Liverpool itakapoikaribisha AC Milan ya Zlatan Ibrahimovic.Kiboko ya makipa Ulaya, Erling Haaland na Borussia Dortmund ataanzia ugenini kwenye mchakamchaka wa kutetea Kiatu cha Dhahabu cha Ligi ya Mabingwa Ulaya, wakati watakapocheza na Besiktas, huku Sporting Lisbon itakuwa nyumbani kucheza na Wadachi Ajax Amsterdam.Mechi nyingine kwenye usiku huo wa Ulaya ni pale FC Sheriff itakapokuwa na kasheshe la kuikabili Shakhtar Donetsk, huku mabingwa wa soka wa Italia, Inter Milan watakuwa na shughuli nzito ya kumkabili Karim Benzema na jeshi la Real Madrid kwenye mchakamchaka huo huko San Siro. Macho ya wengi yanasubiri kuona kile ambacho wachezaji wakali barani Ulaya watafanya kuzisaidia timu zao kwenye hatua hiyo ya makundi.