Kane kitaeleweka tu Man City
MANCHESTER, ENGLAND. NDO hivyo. Manchester City imeamua kuendelea na mchakamchaka wa kufukuzia huduma ya straika Harry Kane kwa muda wote wa dirisha la usajili litakapokuwa wazi hadi hapo litakapofungwa.
Mabingwa hao wa Ligi Kuu England wanaamini kwamba Kane mipango yake ni kuachana na Tottenham Hotspur kwenye dirisha hili la uhamisho wa majira ya kiangazi na kutokana na hilo wanamtaka nahodha huyo wa England atue kwenye chama la Pep Guardiola.
Matumaini ya Man City ni kulipa ada chini ya Pauni 100 milioni kunasa huduma ya Kane na wanaamini Spurs watakubali akakipige Etihad katika dili litakalohusisha pia kubadilishana wachezaji.
Mwenyekiti wa Spurs, Daniel Levy amezidi kuweka ngumu kwamba supastaa wake huyo hauzwi kwa gharama yoyote ile, lakini huko Etihad wao wanaamini dili hilo litatiki tu.
Man City wanaamini matamanio ya Kane kuachana na Spurs yatakuwa rasmi kabla ya dirisha la usajili kufungwa Agosti 31.
Mpango wa miamba hiyo ya Etihad ni kumwona Kane akiongoza kwenye safu ya ushambuliaji ya chama lao mwanzoni mwa msimu ujao, ambapo mechi yao ya kwanza kwenye Ligi Kuu England watakipiga na Spurs, Agosti 15.
Levy hatapenda kuona anawatibua mashabiki wa Spurs kwa kumwona staa wao kwenye jezi za Man City katika mechi yao ya kwanza ya msimu.